Wednesday 20 May 2015

MAMA, NIGUSE MOYO WANGU - SIMULIZI YA HIJA YA LURDI

Hii ni sanamu maarufu sana ya mama Bikira Maria katika maeneo mengi na hasa Tanzania. Ni sanamu ya Bibi yetu wa Lurdi, Mkingiwa dhambi ya Asili.
Lourdes- Ufaransa


Miaka kadhaa imepita tangu nilipofanya hija kwenda  sehemu ya kuhiji kati ya maeneo makubwa zaidi duniani ambayo mama Bikira Maria alitokea mara kadhaa na kufanya miujiza mingi ikiwemo kuponya wagonjwa. Mji huu unaitwa Lourdes ni mji ulipo katika nchi ya Ufaransa ambapo mama Bikira Maria alimtokea msichana maskini Bernadeta Subirou.  Tunaambiwa kwamba, kati ya records za uponyanyaji zilizopo, Lourdes (Lurdi) inaongoza kwa idadi ya uponyaji. Ingawa Mt. Bernadetha hakuahidiwa maisha marahisi hapa duniani, basi sasa anafurahi mbinguni kama Mtakatifu lakini pia, mwili wake haujaoza toka alipokufa mwaka 1879 hadi leo hii.

Mt. Bernadeta Soubirous 




Siku kadhaa zilizopita, Fr. Richard Matanda (Napenda kumuita mtume  wa mama Bikira Maria kwani naona jinsi anavyompenda na anavyoeneza ibada ya mama huyu mwema kwakwe ndio maana nimependa kumuita hivyo) aliniomba niweze kuwashirikisha watu hasa wale wanaofuatilia makala zake kumuhusu mama, juu ya safari yangu ya hija huko Lurdi Ufaransa.




Safari hiyo niliifanya mwaka 2009 wakati huo nilikuwa nikiishi katika nchi ya Uswiss na nchi hii ilipakana sana na nchi ya Ufaransa ingawa safari ya kwenda Lurdi kwa treni ni safari ya siku nzima. Hata hivyo, sikuchukua hatua yoyote ya kutembelea eneo lile. Pengine nilidhani hija ni kwaajili ya watu fulani na sio mimi, pengine ni kwaajili ya watu wenye magonjwa na udhaifu fulani wa kimwili na sio mimi. Kwakweli sababu kubwa ya kutokwenda sikuijua. Kuna siku niliwaza sana nikamwambia mama Maria kwamba nikirudi likizo nitakuja kukutembelea. Mwezi July mwaka huo huo 2009 nilirudi Tanzania kwa likizo kwa muda wa mwezi mmoja na niliporudi kazini kwangu huko Uswisi safari hii nilifikiria sana kuhusu Lurdi lakini sikupata jibu. Kila mara mimi na rafiki zangu tulipanga kutembelea mji huu au ule lakini sikuwahi kusema Lurdi.




 
Vincenza- Marie bele ya mojawapo ya makanisa ya Lurdi 



Siku moja, nikakumbuka ile ahadi yangu ya kwenda hija lakini sikutaka kwenda na ukikumbuka kwamba marafiki zangu wengi walikuwa aidha wapagani au Wakristu wasioamini tena, ilikuwa ngumu kupata  rafiki wa kwenda nae. Basi baana ya kuona wazo lile linaninagi sana, nikamwambia mama " Ukinipa malaika wa kwenda naye, nitakwenda." Siku hiyo jioni nilikutana na rafiki yangu mmoja niiyeishi naye sehemu  moja. Rafiki yangu aliitwa Gisselle (Gisela kwa Kiswahili) yeye alitoka nchi ya Benin na alikuwa akiongea Kifaransa vizuri sana. Sikumbuki tuliongea nini ila nikasema natamani kwenda Lurdi, akasema hata mimi twende wikendi hii.



Vincenzia- Marie na Gissele wakiwa Lurdi



Basi hivyo ndivyo mama alivyonipa malaika wa kwenda naye huko Lurdi. Tulitafuta hoteli tukafanya booking na vilevile tulinunua tiketi za treni tayari kwa safari. Tuliondoka Ijumaa usiku wa saa 4 na  tuliwasili Lurdi saa 12 kamili asubuhi.  Tulienda hotelini  kuoga kisha tukateremka kwenda eneo la tukio. Lurdi ina maeneo kadhaa ya kutembelea lakini maeneo makubwa sana na yanayojaa watu ni yale ya Pangoni mahala aliposimama kabisa mama Bikira Maria na kwenye visima vya  kuoga katika maji ambayo yalitokea baada ya mama Bikira Maria kumwambia atafune majani machungu na kuyatema kisha ikatokea chemchem ya maji, kisha, mama B. Maria akasema  watu wanywe yale maji na wanawe uso watapona. Basi serikali ya ufaransa ikajenga  visima vya kuoga na  sehemu ya kuchota maji. Pia kuna makanisa, njia ya msalaba n.k . Lakini sehemu hizi za pango na Visimani foleni yake huwa ndefu sana na watu hujihimu asubuhi mno. Hatukuwa na muongoza msafara so tukajifanyia safari wenyewe kuanzia kanisani, njia ya msalaba na kanisani tena. Kuna makanisa makubwa kama matatu hivi.

Njia ya Msalaba

Njia ya Msalaba

Njia ya Msalaba

Njia ya Msalaba







Lakini, malaika wa mama Bikira  Maria hakuwa Gisselle peke yake. Kanisani hatukuelewa sana zaidi ya ufafanuzi wa vipeperushi ambavyo Gisselle alinitafsiria. Tulipotoka kanisani, tulikutana na mama mmoja akiwa ameshika bendera. Tulimsalimu mama yule  na kumuomba kumsaidia kushika bendera. Kisha Gisselle akamuuliza unasubiri nini?  akajibu wahujaji wapo kwenye kikundi mimi ni muongozaji wao. Basi nasi tukakaa nae hapo akatuelezea historia nzima kisha akasema tukae pale tuwasubiri wahujaji ili tuweze kwenda nao. Tuliona bahati iliyoje kwani mstari wa kuingia pangoni ulikuwa ni mrefu sana. Basi walipokuja wahujaji wengine tukaongozana, ajabu ni kwamba sisi hatukupanga foleni, tulifunguliwa geti tukaingia pangoni. Lakini  wakati naondoka Uswiss, nilikuwa nina maombi mengi sana na niliyaandika kwenye karatasi. Karatasi kubwa ilijaa huku na huku na bado nikadhani haitoshi lakini niliposogea eneo la hijani nikamwambia mama " Mama mpenzi, nina maombi mengi sana hata wewe unayaona, yote haya ni ya muhimu lakini ombi langu ni moja tu mama, "NIGUSE MOYO WANGU" Sasa hata niliposogea karibu na Pango, nilimwambia mama kwamba  "NIGUSE MOYO WANGU".



Pangoni
 



Tulipoingia pangoni nilipatwa na hali ambayo siwezi kuielezea, nilimfwata polisi na kuomba kupiga picha lakini mikono yangu haikuweza ilitetemeka tu, sikusikia wala kuona watu wengine nilijihisi nipo mimi tu, kiukweli siwezi kuelezea hali iliyonipata. Uso wangu ulijaa machozi na sikuweza kufanya chochote. Tulipotoka Pangoni, yule kiongozi akamwambia rafiki yangu kwa kifaransa Votre ami a reçu la bénédiction" kwamba "Rafiki yako amepokea neema/ benediction". Maneno yale sikuyaelewa mwanzoni lakini baada ya safari yote na kutafakari nilitambua kwamba mama Maria alinipa zawadi niliyomuomba ya kunigusa moyo wangu.
Kesho yake tulibahatika kuoga katika mabafu yale na niliombwa kuanzisha rozari wakati tunasubiria foleni. Nilifanikiwa kupata Sakramenti ya kitubio na kusali misa kisha usiku wa Jumapili tulipanda Treni kurudi Geneva tulipokuwa tukiishi na kuwasili Jumatatu asubuhi. Kwakweli nina mengi ya kueleza lakini haya machache naamini ni zawadi tosha.






Kijito alichovuka Bernadetha kwenda kumuona mama Bikira Maria Pangoni. Njia ya Pangoni na Visima vya kuoga





Pd. Matanda na marafiki wote, simulizi hii ni zawadi yangu kwenu. Mbarikiwe sana

Kwa upendo wa Kristu,

Vincenzia- Marie
 



No comments:

Post a Comment